Sunday, December 10, 2023

SERIKALI YATOA MIL. 114/- KITUO CHA AFYA MTAE, MSD YAKIKABIDHI VIFAA TIBA

Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango, akimpatia nyaraka mbalimbali, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae kilichopo Lushoto mkoani Tanga, Shafii Makamba (kulia), wakati wa makabidhiano ya vifaa tiba vyenye thamani ya Sh.Milioni 114 zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya kununulia vifaa hivyo kupitia MSD kwenye tukio la makabidhiano lililofanyika Disemba 9, 2023. Wengine wanaoshuhudia tukio hilo kutoka kushoto ni Dereva wa MSD, Rashidi Msambo na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama. 

.........................................................

Na Dotto Mwaibale, Lushoto

SERIKALI imetoa Sh.Milioni 114 kwa Kituo cha Afya  Mtae kilichopo Wilaya ya Lushoto mkoani Tanga ambazo zimetumika kununulia vifaa tiba kupitia Bohari ya Dawa (MSD) na hivyo kinatarajia kuanza kutoa huduma ya upasuaji mwishoni mwa mwezi Disemba 2023.

Hatua ya kituo hicho kuanza  kutoa huduma hiyo inatokana na maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya kuibadilisha zahanati ya kijiji cha Mtae kuwa Kituo cha  Afya ili wananchi waweze kupata huduma bora na karibu.

Mganga Mfawidhi wa kituo hicho,  Shafii Makamba akizungumza wakati akipokea vifaa hivyo kutoka MSD alianza kwa kuishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassani kupitia MSD kwa kuwezesha kutoa vifaa hivyo vya dharura kwa ajili ya kufanya huduma ya dharura kwa wakina mama na watoto.

"Vifaa hivi tulivyovipokea leo kutoka MSD Kanda ya Tanga  vitasaidia kupunguza vifo vya wajawazito na watoto kwa sababu kabla ya hapo walikuwa wakilazimika kutembea umbali usiopungua kilometa 65 kwenda Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kupata huduma za dharura hasa za upasuaji na kuwa wataachana na adha hiyo na kupata huduma hii hapa hapa katika kituo chetu," alisema Makamba.

Afisa Huduma kwa Wateja wa MSD Kanda ya Tanga, Mary Isango akizungumza wakati akikabidhi vifaa hivyo kwa niaba ya Meneja wa MSD wa kanda hiyo, Sitti Abdulrahman, alisema wamepeleka vifaa hivyo baada ya kituo hicho cha afya kujengwa jengo la upasuaji na kupelekewa vifaa hivyo vyenye thamani ya Sh.Milioni 114 ambavyo vinaenda kuondoa changamoto waliyokuwa wakiipata wananchi kwenda kupata huduma hiyo mbali.

"Huduma za upasuaji sasa zitafanyika katika kituo hiki baada ya kupata vifaa hivi ambavyo ni muhimu sana sisi kama bohari ya dawa wito wetu kwa watendaji wa kituo hiki ni kuvitunza ili viweze kudumu muda mrefu na kuleta tija kwa wananchi kadri watakavyokuwa wakiendelea kuvitumia kwa kuzingatia kuwa Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuvinunua," alisema Isango.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mtae, Beatrice Alphonce, Disifa Mdoe na Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Andrew Kilama waliishukuru Serikali kupitia MSD kwa kuwapelekea vifaa hivyo ambavyo vitaondoa kabisa madhira waliyokuwa wakiyapata na wakati mwingine kusababisha vifo.

"Tulikuwa na changamoto kubwa baadhi ya wajawazito walikuwa wakijifungulia njiani kutokana na umbali mrefu wa kwenda Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kupata huduma lakini sasa tutakuwa tunaipata hapahapa nyumbani kwa kweli tuna kila sababu ya kumshukuru Rais wetu mama Samia kwa kutuona na kutuonea huruma wanawake wenzake na kama ingewezekana tungemuomba siku moja aje hayaone kwa macho maendeleo haya aliyotuletea," alisema Alphonce.

Alphonce alitumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Samia, Mbunge wa jimbo hilo, Rashid Shangazi na viongozi wa wilaya hiyo kwa jitihada kubwa wanayoifanya ya kuwaletea maendeleo hayo ambapo aliwaombea kwa Mungu awape afya na maisha marefu.Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae, Shafii Makamba wakizipitia nyaraka hizo kabla ya kukabidhiana vifaa hivyo.Mapitio ya nyaraka hizo yakifanyika kwa pamoja kabla ya makabidhiano. Kutoka kushoto ni Afisa Huduma kwa Wateja wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Tanga, Mary Isango, Dereva wa MSD, Rashidi Msambo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama na  Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Kijiji cha Mtae, Shafii Makamba,Mwenyekiti wa Kijiji cha Mtae, Andrew Kilama akishukuru Serikali kwa kuwapelekea vifaa hivyo kupitia MSD,Muonekano wa Zahanati ya Kijiji cha Mtae kabla ya kubadilishwa kuwa Kituo cha AfyaMuonekano wa jengo la upasuaji lililojengwa na Serikali na kuipandisha hadhi zahanati hiyo kuwa Kituo cha Afya.Vifaa tiba hivyo vikitolewa kwenye gari tayari kwa makabidhiano.Vifaa tiba vikipelekwa kwenye jengo la upasuaji.Watoto wa Kijiji hicho wakishiriki kubeba vifaa hivyo.Kazi ya ubebaji wa vifaa hivyo ikiendelea.Vifaa vikibebwa.Wananchi wa kijiji hicho wakishiriki kubeba vifaa hivyo.Mkazi wa kijiji hicho, Beatrice Alphonce akiishukuru Serikali na MSD kwa kufanikisha kupatikana kwa vifaa hivyo.Mkazi wa kijiji hicho, Disifa Mdoe akipipongeza Serikali na MSD kwa kuwapelekea vifaa hivyo.Gari la MSD likiwa safarini kupeleka vifaa hivyo.

Monday, December 4, 2023

REA YAWASHA MRADI WA BILIONI 25 KUPOZA, KUSAMBAZA UMEME IFAKARA MOROGORO

Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya, akizungumza baada ya kuwasha  Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara    (Ifakara Substation), Desemba 3, 2023 Ifakara, Morogoro. Kituo kimejengwa na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) kwa gharama ya Shilingi bilioni 25.

...........................................................................

Na Mwandishi Wetu, Ifakara-Morogoro

SERIKALI  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) imewasha Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha  Ifakara ambacho kimegharimu shilling bilioni 25.

Akiwasha kituo hicho ambacho kimelenga kuongeza uwekezaji na uanzishaji wa viwanda kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero , Mh Dunstan Kyobya ameshauri kituo hicho kiitwe Samia Ifakara Substation.

Ameipongeza REA na EU kwa kuhakikisha kituo kimekamilika na kuwashwa kwani kinaenda kumaliza matatizo ya umeme katika wilaya ya Kilombero, Malinyi na Ulanga ambayo ni maeneo ya kimkakati ya kilimo na viwanda.

“Tunategemea kuongeza uwekezaji kwa kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na vile vya kuchakata madini” amesema Mh Kyobya.

Amewataka wananchi kuhakikisha wanatunza mazingira na vyanzo vya maji ili kujihakikishia umeme wa uhakika katika mabwawa ya kuzalisha umeme ya Kihansi na Kidatu.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Jones Olotu amesema kuwashwa kwa kituo hicho kunaongeza upatikanaji wa umeme na hivyo kuwawezesha wananchi  kukuza na kuboresha hali zao za kiuchumi kwa kufungua biashara mbalimbali kwa uwepo wa umeme wa uhakika katika maeneo hayo.

“Wananchi watumie upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa kujiongezea kipato kwa kuwekeza na kuanzisha viwanda vya mazao ya kilimo na madini ambayo yanapatikana kwa wingi Kilombero, Ifakara, Ulanga na Malinyi,” amesema Mhandisi Olotu.

Naye Mbunge wa Kilombero, Aboubakar Asenga amewataka wananchi wa Jimbo hilo kuchangamkia fursa ya upatikanaji wa umeme mkubwa kwa kuzalisha kwa wingi na kuanzisha viwanda vikubwa.

“Tunaishukuru serikali kwa kutimiza ahadi yake, ni wajibu wetu wananchi kutumia fursa hii ya upatikanaji wa umeme mkubwa kwa kuwa na viwanda vya kukausha na kukoboa mpunga, uzalishaji wa matofali kwa kisasa na uongezaji thamani wa madini ili kujiongezea kipato, ” amesema Mh Asenga.

Meneja wa Mradi huo kutoka REA, Mhandisi Romanus Lwena amesema ujenzi wa kituo hicho ulianza 2020 ambapo kinazalisha kV 220 za umeme baada ya wananchi wa maeneo hayo kuwa wanapata umeme mdogo wa kV 33 uliokuwa unasababisha kukatika mara kwa mara.

Na baada ya kuwashwa kwa kituo hicho, kutawezesha kuwa na umeme wa uhakika kwa ajili ya viwanda na shughuli nyingine za kilimo.

Meneja Miradi ya Nishati wa EU, Mhandisi Francis Songela amesema katika Mradi huo wamechangia shilingi bilioni 18 na Serikali ya Tanzania imetoa shilingi bilioni 7.

Amesema kituo hicho kipo katika eneo la  kimkakati la  Mpango wa Kukuza Kilimo Ukanda wa Kusini mwa Tanzania , SAGCOT ambapo Mradi huo unaenda kuleta mapinduzi ya kilimo na viwanda.

“Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi ni maeneo ya kimkakati ya SAGCOT kwani yana rutuba kwa kilimo na shughuli nyingi za kiuchumi ambapo umeme wa uhakika ilikuwa changamoto  na kwa kuwashwa kwa kituo hiki tunategemea mapinduzi ya kilimo na viwanda, ” amesema Mhandisi Songela.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Jones Olotu akizungumza.
. Mbunge wa Kilombero, Mhe. Aboubakar Asenga akizungumza.
 Meneja wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation) kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Romanus Lwena akitoa maelezo kuhusu Kituo hicho kwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya na Viongozi wengine mbalimbali wakati wa tukio la kuwasha Kituo hicho kilichojengwa na Serikali kupitia REA kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU) kwa lengo la kuimarisha huduma ya upatikanaji umeme kwa wananchi wa wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi.
Taswira ya Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation). Taswira hii ilichukuliwa Desemba 3, 2023 wakati wa tukio la kuwasha rasmi Kituo hicho baada ya ujenzi wake kukamilika.
Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dunstan Kyobya (katikati)  akiwa pamoja na Viongozi mbalimbali na wataalam kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), TANESCO na Umoja wa Ulaya (EU) wakifurahi baada ya tukio la kuwasha rasmi Kituo cha Kupoza na Kusambaza Umeme cha Ifakara (Ifakara Substation), Desemba 03, 2023.